Breaking News
Loading...
Sunday, 28 September 2014

Info Post


        Hakika nyakati zinapita na muda unakwenda, majira yanabadilika na miaka inakwenda au kwa namna nyingine umri wako na wangu unakua. Umri unavyozidi kwenda basi  uwezo na utambuzi wa vitu au uelewa wa mambo unakua kwa haraka sana ila kama tu utaruhusu mwili ukue pamoja na akili. Malezi uanzia kwa wazazi wetu pamoja na jamaa zetu ambao wanatulea huku katika jamii zetu. Kwa nyakati zetu tulielekezwa vitu vingi sana japo siyo vyote kwa mfano kuweza kukadiria muda kwa kulitazama jua au kuweza kujua mahala au uelekeo yani kaskazini au kusini kwa kuangalia nyota wakati wa usiku. Naamini haya yalikuwa baadhi ya mafundisho kutoka kwenye simulizi za mababu zetu au nyanya wetu.
        Kwa vijana wa enzi za analojia ni tofauti sana na dijitali, kwasababu vijana wa analojia wanajua nini maana ya kutandika na kutandua mkeka chini ya mti au miti iliopo mbele ya nyumba yao hasahasa wakikimbilia nafasi za mbele kusikiliza simulizi za mababu yani hadithi zenye mafundisho mengi sana kama methali, vitendawili na nahau au misemo mbalimbali. Subira yavuta kheri, au mvumilivu hula mbivu, vipi unazikumbuka hizi. Najua unatabasamu, ndio haya ni baadhi ya maneno ya wahenga tu.
        Wahenga wanawashangaa sana viongozi na baadhi ya walimu wa mpira wa Tanzania na huku wakijiuliza maswali mengi sana kama kweli hawa walimu walitandika na kutandua mikeka ili kusikiliza simulizi zao, najua wanaumia sana na mioyo yao inanung’unika sana wakihofia kwamba hawa walimu na viongozi wa soka letu ni kweli wanakumbuka simulizi zao au wanazikumbuka lakini wameamua kupuuzia tu. Na maswali yao mengi ni kwamba ,  hata kama wanazikumbuka kwanini basi hawatumii utaalamu wa kusoma muda kwa kuangalia jua au kuishi kwa kulingana na nahau na misemo yao yenye mafundisho.
         Kipenga cha ligi ya Tanzania bara kipeshapulizwa kuangalia ni nani atakabidhiwa kombe na wanalambalamba yani Azam Fc au wanalambalamba hao watajitetea na kulitunza tena kombe lao katika mifuko yao ya Azam. Viongozi wa vilabu tofauti vya ligi yetu wanashindwa kabisa kutofautisha uzoefu, ubunifu na ujuaji, na matokeo yake wanapingana na methali ya “subira yavuta kheri au “mvumilivu hula mbivu” na hapo ndipo wanapowakasilisha wazee wa simulizi za mikeka na kuamua kuitupa au kuificha mbali mikeka yao. Matokeo ya haya yote pamoja na kukosa somo la kutofautisha vitu hivyo vitatu wanaamua kuchagua au kubadili makocha wa vilabu vyao kwa kusikiliza ufundi wa mdomoni au ujuaji na kuacha kuangalia swala la ubunifu na uzoefu.
          Msimu wa ligi ilyopita yani msimu uliopita tulishudia kufukuzwa au wenyewe wanaita kubadili kwa makocha wa timu kumi na mbili tofauti za ligi yetu na kuziacha timu mbili tu ambazo wahenga wanaamini viongozi wa timu hizo ndio waliotandika mikeka wakati wa umri wao nazo ni Mtibwa Sugar na Mbeya City na walimu wao Juma Mwambusi na Meckie Mexime. Viongozi wa timu hizi walikuwa na staha na heshima na kuelewa kuwa kila kitu kizuri kinahitaji muda na nafasi nzuri bila msukumo wa kishabiki au maslahi binafsi, naamini wote tulishuhudia viwango vya timu hizi mbili japo hazikufanikiwa kuchukua ubingwa.
             Hivi kwanini viongozi wa vilabu vya Tanzania wasimuangalie kocha mzuri kwa kutazama mbinu zake, uwezo wake na ubunifu wake katika mpira na waache kuangalia uwezo wa kocha kwa kutazama au kwa kusikiliza mazungumzo yake hasa akielezea mfumo wake wa uwanjani. Kwa muelekeo wa hivi sasa hata wewe ukiwa muongeaji mzuri na unamfahamu hata mjumbe mmojawapo katika kilabu husika basi utapewa nafasi ya kuwa kocha wa timu hiyo. Ifike wakati viongozi wa vilbu tofauti wawe na subira na heshima kwa makocha wa vilabu vyao kwa kuwaamini na kuwapa motisha mi naamini watashinda tu japo katika ushindani lazima kila nafasi iwe na mwenyewe kuanzia mshindi mpaka anayeshuka daraja.
          Umefika wakati walimu wa soka letu na viongozi wa vilabu vyetu kutandikiwa mkeka na kusikiliza simulizi za mababu zetu ili wajikumbushe busara na maneno yenye mashiko ili wavitumie katika mpira na kuacha kuwanyayasa makocha kwa kujifanya wao ni wajuaji. Wafundishwe kujipenda na kujijali wao kwanza na siyo kuwapa nafasi kwa kiasi kikubwa makocha wa kigeni kuja kufundisha vilabu vyao kwa hofu zao tu, wakati kuna watu kama Mbwana Makata, Abdallah Kibaden ,Hemedy Morocco na wengine wengi ambao wakifanya masomo kidogo, na elimu nzuri kwa nadharia ya vitendo wanaweza kuwa walimu wazuri sana na wakutumainiwa hasa tu wakiaminiwa. Kilichobaki ni kuifuma mikeka na kuandaa vipaza sauti tayari kwa simulizi au hadithi za wahenga.  

                                   Na,
                                         Kelvin Kiimbila Jr
                                         0719580495
                                        Kmichel350@gmail.com / Ngotejr@gmail.com