Breaking News
Loading...
Monday, 2 March 2015

Info Post


MWADUI IMEPANDA SHUGHURI IMEIVA
Nimesoma Mwadui,nimekulia Mwadui nimecheza mpira Mwadui naijua vizuri Mwadui ,ukifika Mkoani Shinyanga unatoka kidogo nje ya mji kama unaenda Mwanza unapita vitongoji vya Korandoto na Maganzo mbele kama mita tano hivi unapinda barabara upande wa kulia  unakutana na geti kubwa la kuingia katika Mgodi wa Mwadui unaojishugulisha na kuchimba Almasi, ni Mgodi  ambao bado ndungu zetu wa Afrika kusini bado wana hisa yao katika Mgodi huo ambao ulivumbuliwa Williamson.
Mwadui ni eneo ambalo mambo unayo yasikia kule Ulaya yalikuwepo Mwadui wakati nikiishi kule miaka ya 70 hadi ya 80 ,ilikuwa tunaishi maisha kama hauko Tanzania, sina hakika na leo ,wachezaji wa Mwadui enzi hizo tulikuwa tunalelewa kama tupo Ulaya katika Hostel ya Uhuru , Mwadui ndio timu pekee miaka ile ilikuwa ikisafiri kwa Ndege kwenda sehemu yeyote kucheza soka,ina Super Market kubwa mno sijapata kuona enzi zile, ni sehemu pekee miaka ile matumizi ya pesa ya cash ilikuwa si muhimu kama ilivyo leo Mitandao ya tigo pesa na M pesa inavyotufanya tusitembee na hela,ina viwanja bora na vingi vya kufanyia mazoezi kuanzia vile vya maeneo ya Posta hadi Compaund,wachezaji walikuwa hawana kabisa matatizo ya kula ,kulala,  matibabu wala vifaa.
Kwa mazingira hayo Mwadui mbali ya kutoa timu nzuri na  wachezaji wenye kuleta upinzani mkubwa katika soka letu miaka ile bado iliweza kuibua kocha iliyepata kufundisha timu ya Taifa akitokea Mwadui Mzee Elijah Kategile,ni moja kati ya makocha waliotupeleka hadi kwenye Mataifa huru ya Afrika akishirikiana na Mh Joel Bendera na Mohamedy Msomali ambayo hadi leo bado tunayatolea macho.,Mwadui iliweza kuleta wachezaji katika timu ya Taifa kama akina Joseph Mbelwa maarufu kama Bagina,Zuberi Kaiwanga,Hamis Kamaka,James Ngo’nga,Ahmedy Abasi ,David Mwakalebela ,Justine Simfukwe na wengineo
Lakini Mwadui imewahi kuwa na wachezaji zaidi ya hao ambao walikuwa maarufu na hawakucheza timu ya Taifa kama akina John Lega ,Rwemaho Mkama, Benard Madale,Anko Shubetr,Chia Masonga,Wagadugu,Tostao,Ally Bushiri,Deus Kapandila,Masolwa ,Yona Kiombo,Mkama Ntale,Aman Rashid,Ally Bushiri na wengine wengi tu.
Chimbuko la wachezaji hao ni utaratibu mzuri wa mashindano yao ya ndani ambayo yalikuwa yanashikrikisha timu za Idara kuanzia ile ya Mji,Uhandisi,Uzalishaji ,Utawala hadi Almas na mgeni rasmi wa kukabidhi kombe na zawadi alikuwa akitoka Afrika kusini na ndio ilikuwa chachu ya kupata wachezaji wa kuunda timu ya Mwadui.
Leo Mwadui ile ninayoifahamu mimi kama ndio yenyewe ambayo imepanda daraja chini ya kocha mwenye mbwembwe nyingi hapa nchini lakini pia akiwa na mafanikio mazuri tu ya soka Jamuhuri Kiwhelu maarufu kama  Julio,naamini kutakuwa na shughuri pevu msimu ujao.
Kocha Jamuhuri Kiwhelu  ni moja kati ya makocha wazalendo wanaoujua vizuri mpira na mashindano ya nyumbani kwetu,anamjua kila mtu aliye wa mpira na hata Yule anayejiita mtu wa mpira,Julio ni mpambanaji ni mpenda sifa asiyekubali kushindwa lakini cha zaidi ni msema ukweli na hafichi kutoa hisia zake hivyo hata kama kuna watukama wanataka kumuharibia matokeo hatakaa kimya atapiga kelele tu na watu tutaona kuwa hapana hapa Mwadui wanaonewa, Julio analijua soka letu.